TMA YATOA MWELEKEO WA MVUA MSIMU WA NOV 2024 HADI APR 2025

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang'a wakati akitoa taarifa kwa wanahabari kuhusu mwelekeo wa msimu wa mvua Novemba 2024 mpaka April 2025.
.......................

NA MUSSA KHALID

Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini Tanzania –TMA imesema katika msimu wa mvua za Novemba 2024 mpaka April 2025 zinatarajiwa kuwa za wastani hadi chini ya wastani katika maeneo mengi ya kanda za Magharibi.

Imesema mvua hizo ni mahususi kwa mikoa inayopata msimu mmoja wa mvua kwa mwaka kanda ya magharibi,kati, nyanda za juu kusini magharibi, kusini mwa nchi, ukanda wa pwani ya kusini pamoja na maeneo yaliyopo kusini mwa mkoa wa Morogoro.

Hayo yameelezwa jijini Dar es salaam na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang'a wakati akitoa mwelekeo wa msimu wa mvua Novemba 2024 mpaka April 2025.

‘Aidha, kwa maeneo ya kanda ya Ziwa Victoria mvua zilitarajiwa kuwa za Wastani hadi Chini ya Wastani. Msimu wa Vuli, 2024 ulitarajiwa kutawaliwa na vipindi virefu vya ukavu na mtawanyiko wa mvua usioridhisha. Aidha, mvua hizo zilitarajiwa kuanza kwa kusuasua wiki ya nne ya mwezi Septemba, 2024 katika ukanda wa Ziwa Victoria na kusambaa katika maeneo mengine yanayopata mvua za Vuli kati ya wiki ya pili na ya tatu ya mwezi Oktoba, 2024’amesema Dkt Chang’a

Aidha Dkt Chang’a amesema katika msimu huo Vipindi vya unyevu wa kuzidi kiasi pamoja na mafuriko vinaweza kujitokeza na kuathiri ukuaji wa mazao kwa maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani.

Amewashauri Wakulima kuandaa mashamba, kupanda, kupalilia na kutumia pembejeo husika kwa kuzingatia hali ya unyevu katika udongo, kutumia mbinu bora na teknolojia za kuzuia maji kutuama shambani, kuhifadhi maji shambani, kuzuia mmomonyoko na upotevu wa rutuba kutokana na kutuwamisha maji kwa muda mrefu au mafuriko.

Awali akitoa tathmini ya mvua za msimu uliopita Mtaalamu wa Hali ya Hewa kutoka Mamlaka ya Hali ya hewa Tanzania (TMA) Rose Senyagwa amesema maeneo mengi yanayopata mvua za msimu mmoja kwa mwaka yalipata mvua za juu ya wastani isipokuwa maeneo machache.

Hata hivyo Mamlaka hiyo imewashauri wadau wa Sekta Binafsi kushirikiana na wataalamu mbalimbali ikiwemo wataalam wa hali ya hewa ili kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza katika wakati huo wa msimu wa mvua.

Post a Comment

Mpya zaidi Nzee zaidi